Tuesday, September 3, 2013

KASHFA YALIKUMBA JESHI LA POLISI TENA-CCTV ZAZIMWA KURUHUSU UJAMBAZI

SIKU chache baada ya tukio la wizi mkubwa wa fedha katika Benki ya Habibu mjini Dar es Salaam, siri nzito zimeanza kuvuja kuwa polisi wanadaiwa kuhusika katika tukio hilo kwa kuhujumu kamera za usalama za CCTV zinazomilikiwa na jeshi hilo. 

Katika tukio hilo, watu wanaodaiwa kuwa majambazi walipora dola za Marekani 20,000 ambazo ni sawa na Sh milioni 32 za Tanzania.

Katika tukio hilo, Polisi Mkoa wa Ilala inamshikilia askari mmoja kwa kosa la kuhusika katika tukio hilo kutokana na kushindwa kuchukua hatua za haraka wakati tukio linatokea.

Habari za uhakika kutokana ndani ya jeshi hilo, zinasema siku ya tukio polisi waliokuwa zamu kuongoza mitambo hiyo, kwa namna moja au nyingine wanadaiwa kufanya hujuma hiyo, kwa lengo la kupoteza mawasiliano na maeneo mengi ya polisi.

Chanzo chetu hicho, kiliongeza kuwa siku ya tukio eneo lote la mzunguko wa barabara ya Uhuru na maeneo ya jirani na Kiwanda cha Bia Tanzania (TBL), sehemu zote hazikuwa na huduma ya kamera za usalama, jambo ambalo si la kawaida kutokea.

“Hatua iliyofikia sasa ni mbaya, huwezi amini siku ya tukio kamera za CCTV zinazotumiwa na polisi zilizimwa kabisa, kitendo hiki kilisababisha polisi makao makuu wasijue nini kinachoendelea pale.

“Ndiyo maana utaona kuna askari mmoja anashikiliwa katika tukio lile, haiwezekani kituo kikuu kishindwe kubaini uwapo wa tukio hili, wakati kuna mawasiliano ya kutosha, umefika muda wa kulisafisha jeshi letu kwa kasi,” kilisema chanzo chetu.

Chanzo hicho, kilisema mitambo ya kamera hizo, ilizinduliwa na Rais mstaafu Benjamin Mkapa mwaka 2004 na imekuwa ikifanya kazi bila matatizo yoyote.

“Nimekuwapo hapa tangu mwaka 2004, kamera hizi zilipozinduliwa rasmi na hazijawahi kuharibika hata siku moja, iwe siku ya tukio zisifanye kazi,” kilihoji chanzo chetu.

Askari aliyekamatwa katika tukio hilo, anadaiwa anafanya kazi katika kituo cha Oysterbay Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Marietha Minangi, alithibitisha kukamatwa kwa askari huyo.

Kamishna wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova alipoulizwa na MTANZANIA jana, alisema ameipokea taarifa hiyo na wanaifanyia kazi haraka iwezekanavyo.

“Taarifa hii tumeipokea, tunaifanyia kazi haraka sana ili kupata ukweli, naomba tuwe na subira,” alisema kwa kifupi Kamishna Kova.

Alisema bado polisi wanaendelea na uchunguzi wa tukio hilo na kwamba watu waliokamatwa watafikishwa mbele ya vyombo vya dola.

No comments:

Post a Comment