Wednesday, November 13, 2013

MBUNGE CHADEMA AENDELEA KUSOTA LUPANGO....FUATILIA ZAIDI HAPA

JUHUDI za kumdhamini Mbunge wa Ukerewe, Salvatory Machemli (Chadema), aliyewekwa mahabusu kwa siku ya nane sasa, zimekwama. Kaimu Hakimu wa Mahakama ya Wilaya ya Ukerewe, Mrisho Abed, alisema jana kuwa amri ya kumweka Machemli rumande kwa siku 14 ilitolewa baada ya mshitakiwa kushindwa kutimiza masharti ya dhamana.


Alisema Sheria ya Makosa ya Jinai namba 20 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002 imeipa Mahakama mamlaka ya kufuta dhamana ya mshitakiwa.

Hakimu Abed ambaye ni Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo ya Bukindo, alisema amri hiyo ilitolewa chini ya sheria hiyo na chombo pekee chenye mamlaka ya kuitengua ni Mahakama Kuu.

Akifafanua zaidi, hakimu huyo alikwenda mbali zaidi na kueleza kuwa kesi hiyo inayosikilizwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Ukerewe, Faustine Kishenyi, ingekuwa chini yake asingetoa dhamana kwa mshitakiwa hadi kesi hiyo iishe.

Alisema Machemli anayekabiliwa kesi ya uchochezi namba 19 ya mwaka huu alifutiwa dhamana Novemba 6 mwaka huu, baada ya kushindwa kufika mahakamani zaidi ya mara tano bila taarifa wakati kesi yake ikitajwa.

Hakimu Abed alisema mbali ya kuruka dhamana mara tano, pia kitendo cha kushindwa kutoa taarifa ni uthibitisho tosha wa kudharau Mahakama na kuongeza kuwa Sheria hiyo inatoa mamlaka ya kufuta kabisa dhamana yake, hadi kesi yake isikilizwe na kukamilika.

Katika utetezi wake, Machemli (39) ambaye kesi yake imepangwa kuendelea kusikilizwa hapo Novemba 20 mwaka huu, alidai alishindwa kufika mahakamani kama ilivyopangwa, kutokana na siku za kesi kuingiliana na vikao vya bunge.

Maelezo hayo yaliwafanya watu waliofika kumdhamini na baadhi ya washabiki wake waliofika mahakamani hapo, kuondoka huku wakitishia kutumia nguvu ya umma kushinikiza dhamana.

-habarileo

No comments:

Post a Comment