Tuesday, January 29, 2013

Wajawazito Mbeya wasukumana kwa wakunga wa jadi kujifungua Chunya

: Kulia ni Mkunga Agripina Sikanyika akimkabidhi mtoto mmoja wa wajawazito waliotoka kujifungua nyumbani kwake
Mkokoteni unaokokotwa na Punda hutumika pia kubebea baadhi ya wajawazito kwenda katika kituo cha afya cha Mbuyuni na kwa Mkunga wa jadi Mama Namwinji
: Mwonekano wa Nyumba inayotumika kujifungulia wajawazito kwa Mkunga Agripina Mama Namwinji.
Mama Namwinji akionesha mkeka aina ya Msengele anaotandika wanapojifungulia wajawazito wanapofika kwake 
KATIKA vijiji vya Totowe na Mbuyuni hakuna serikali. Ni utawala binafsi. Huku ni katika wilaya ya Chunya mkoani Mbeya. 
Kwani Sera ya Afya ya mwaka 2007 inasema wajawazito kote nchini watapata huduma bure kabla na wakati wa kujifungua. Lakini hayo hayaonekani katika vijiji hivyo. 
Pamoja na kuwepo zahanati katika kata ya Totowe, wanawake kwa mamia wanasukumana wakitafuta kupewa huduma ya uzazi kwa wakunga wa jadi ambao serikali haijawatambua. 
Hilda Said Kawinga (80), mkazi wa kijiji cha Malangali mpoa kata ya Totowe ni mkunga kwa miaka 30. Anaishi katika banda la vyumba viwili ambavyo anaita sebule na chumba cha kulala. 
Kwa umri wake Hilda hatetemi mikono. Kwa rekodi za sasa, ameweza kusaidia wajawazito 70 kujifungua katika kipindi cha miezi 10 (Januari hadi Oktoba mwaka 2012). 
Kijiji cha Totowe kipo umbali upatao kilometa zaidi ya 100 kutoka Chunya mjini. Hapa ndipo wajawazito wanaita kwa jina la kirafiki, “nyumbani salama,” kutokana na kujifungua salama na kuondoka kwa kicheko na watoto wao mikononi. 
Hapa ni nyumbani kwa Hilda. Pale kuna mafiga Ndilo jiko. Kuna kuni. Hapa kuna vyombo vya kupikia. 
Alipokaa mwandishi kuna mkeka na ndiyo sehemu inayotumika wakati wa kusaidia wajawazito kujifungua. Wajawazito wakija, basi hakuna mgeni. 
Bibi Hilda hana mkasi. Hana vyombo vya kisasa kama vya zahanati, kituo cha afya au hospitali kwa huduma za uzazi. Hana kitanda. Hana godoro wala mipira ambako wajawazito hujilaza wakati wa kujifungua. 
Lakini hapa ndipo wanawake wanamiminika kwa huduma ya uzazi na wanaondoka na watoto wao salama. 
Akiongea kwa sauti nyembamba anasema, “Ninamworodhesha kila anayejifungulia hapa katika daftari langu. 
Nafanya hivi ili kuisaidia serikali kupata takwimu endapo watazihitaji; ingawa tangu nimeanza shughuli hakuna kiongozi wa serikali aliyewahi kuja kuangalia wala kuuliza kuwa ninafanyaje kazi.” 
Hilda anajigamba kwamba alipata ujuzi kutoka kwa mama na kuongeza, “…kwa watoto wangu sikuwahi kujifungulia hospitali; ilikuwa kazi ya mama. Hapo ndipo nilijifunzia kazi tena bila vifaa vya kisasa. Sharti kuu ni kuwa msafi tu.” 
Hivi sasa anasema anapokea wajawazito 10 kwa mwezi na kila mmoja anaondoka kwa kicheko. Tangu aanze kazi hii, hakuna mtoto wala mama aliyepoteza maisha akiwa mbele yake. 
Bibi Hilda ni kama mkunga mwingine Agripina Frederick Sikanyika wa kijiji cha Mbuyuni wilaya ya Chunya. Tofauti ni kwamba Agripina ametenga nyumba rasmi kwa wajawazito kulala na kujifungulia. 
Agripina, mwenye umri wa miaka 37 anafahamika sana kwa jina la “Mama Namwinji.” Anasema imemlazimu kuwaachia nyumba wajawazito wanaokwenda kwake kwa ajili ya kusubiri kujifungua kutokana na idadi yao kuongezeka kukicha. 
Katika kipindi cha miezi 10, Januari hadi 9 Oktoba 2012, Mama Namwinji amehudumia wajawazito 212. Alianza huduma kwa wajawazito mwaka 2000. 
Kwa Mama Namwinji, idadi ya waliojifungulia mikononi katika kipindi hicho ni rekodi. Mwaka 2011 ni wajawazito 98 waliojifungulia kwake. 
Kitu kimoja kimemkwaza Mama Namwinji.
Watoto wawili kati ya 212 waliozaliwa mwaka jana walikuwa na ulemavu. Ilikuwa Septemba 15, 2012 wakati mwanamke mmoja alipojifungua mtoto mwenye sikio moja, mguu mmoja, mdomo na pua vikiwa vimeungana. Mtoto huyo alifariki muda mfupi baada ya kuzaliwa.
Siku iliyofuata, Septemba 16, 2012 alizaliwa mtoto aliyekuwa na kichwa kikubwa chenye umbile la kichwa cha ng'ombe lakini mwenye kiwiliwili cha binadamu. 
Mkunga amesema hawezi kutoa majina ya waliojifungua “watoto wa ajabu” kwa alichoeleza kuwa ni siri ya wazazi wao na aliyekuwepo.
Changamoto anazokabiliana nazo Agripina hazina tofauti na zile za Bibi Hilda na wakunga wengi wa jadi nchini. Hana kitanda, hivyo huwalaza wajawazito kwenye mkeka wa matete (maarufu kama Msengele). 
“Hii ni hatari kwa sababu wanaweza kupata magonjwa hasa kipindi cha masika,” anasema Agripina.
Kama Hilda, Agripina naye anaorodhesha wajawazito katika daftari maalum, ingawa yeye anachukua hatua zaidi kwa kuangalia kadi za kliniki na kuzijaza mara wanapojifungua. 
Anasema pamoja na kuwepo kwa kituo cha afya jirani cha Mbuyuni (Chang’ombe), lakini wajawazito wengi wanakimbilia kwake kwa madai kwamba wakienda hospitalini wanaweza kufanyiwa upasuaji. 
“Wapo ambao walikwenda hospitalini wakafanyiwa upasuaji, lakini walipofika hapa katika uzazi wao mwingine wameendelea kujifungua bila upasuaji,” anasema. 
Kama ilivyo kwa Bibi Hilda, Agripina naye anasema huwa hatozi kiwango chochote cha fedha kabla na baada ya mjazito kujifungua, ingawa wote wanakiri kwamba akinamama au ndugu zao “…huleta chochote walichojaliwa kama asante.” 
“Wanawake wengi Tanzania wanakufa kipindi cha ujauzito au baada ya kujifungua ndani ya siku 40. Hii ni hatari sana,” anasema Dk. Magoma akiwa anafundisha waandishi wa habari Tanzania wanaobobea katika habari za afya ya uzazi akiwemo mwandishi wa makala haya na kuongeza kuwa, kwa upande mwingine, watoto wanakufa ndani ya kipindi cha miezi sita baada ya kuzaliwa huku akibainisha kwamba asilimia 57 ya wanawake wote wanaojifungua hawahudhurii kliniki. 
Mtafiti wa Masuala ya Afya nchini, Dk. Kahabi Ganka Isangula, anasema zaidi ya wanawake 300,000 wanafariki kila mwaka wakati wa kujifungua au wakati wa kipindi cha ujauzito kutokana na sababu mbalimbali huku 800 kati yao wakifa kwa “matatizo yanayoweza kuzuilika.” 
Kati ya vifo hivyo, asilimia 99 hutokea katika nchi zinazoendelea hasa vijijini kwa watu maskini ambapo wajawazito wengi hutokwa na damu nyingi wakati wa kujifungua. 
Anashauri wanawake wajifungulie katika vituo vya afya akieleza kuwa moja ya changamoto kwa huduma za wajawazito, “ni kutoa kondo la nyuma ambalo linahitaji utaalamu.” 
Hata hivyo, Dk. Isangula hapingi matumizi ya wakunga wa jadi katika kuhudumia wajawazito. Anasema, “…hakuna ubaya wowote kwa wanawake kujifungulia kwa wakunga wa jadi, tatizo linakuja katika upatikanaji wa vifaa vinavyomwezesha mkunga wa jadi kumhudumia mama mjamzito katika hali ya usalama.” 
Naye Mratibu wa Huduma za Afya ya Uzazi na Mtoto kutoka hospitali ya mkoa wa Mbeya, Prisca Butuyuyu, anasema wanatambua kuwepo kwa wakunga wa jadi na kwamba watoto wote wanaozaliwa huko wanawahesabu kuwa wanazaliwa nyumbani kwa sababu hakuna mwongozo wa wizara unaowatambua wakunga wa jadi. 
Sera ya Afya ya mwaka 2007 inaagiza kwamba wajawazito wapewe huduma bure katika sehemu zote za huduma ya afya. Je, hawa wanaojifungulia kwa Hilda na Agripina wanapata huduma gani au huduma inayotajwa haiwahusu? 
Je, kama wajawazito hawapati huduma, wakunga wanasaidiwa vipi au wanawezeshwa vipi na serikali ili wafanye kazi yao kwa ustadi na weledi ambao tayari umedhihirishwa kwa kuhudumia mamia kwa mamia ya wajawazito waliojifungua salama?
Majibu kwa maswali haya yako mikononi mwa serikali

No comments:

Post a Comment