Wednesday, October 2, 2013

SANGOMA ANASWA AKILINDA WAHAMIAJI HARAMU KWA DAWA

Mganga akamatwa na hirizi zenye chura wanaopumua akizitumia kuwauzia wahamiaji haramu wasiweze kukamatwa katika Operesheni Kimbunga.
Kampeni ya kitaifa ya kuwaondoa wahamiaji haramu nchini iliyopewa jina la “Operesheni Kimbunga”, imezidi kuibua mambo mazito baada ya mganga wa kienyeji, kugundulika akitumia uchawi ili kuwalinda wahamiaji hao wasikamatwe.
. Mganga huyo aliyefahamika kwa jina la Bw. Bahalaye Gwenda (60), ameifanya kazi hiyo tangu kuanza kwa operesheni hiyo kwa kuwalipisha wahamiaji haramu sh. 200,000 kila mmoja wasiweze 
kukamatwa na vyombo vya dola vinavyofanya kazi hiyo.
Tukio hilo la kustaajabisha, limetokea katika eneo la Kigaga, Wilaya ya Kibondo, mkoani Kigoma ambapo mganga huyo hutumia hirizi ambazo ndani yake kuna dawa za kienyeji na vyura wanaopumua kuwauzia wahamiaji hao.
Taarifa za mganga huyo, ziliifikia Kamati ya Ulinzi na Usalama wilayani humo ambapo Mwenyekiti wa kamati hiyo Mkuu wa Wilaya hiyo, Bw. Venance Mwamotto, aliongoza kikosi kazi cha wajumbe wa kamati, polisi hadi nyumbani kwa mganga.
Kamati hiyo ilipata malalamiko hayo kutoka kwa wahamiaji ambao walikamatwa mbali ya kupewa dawa na mganga huyo ambaye ni raia wa nchi jirani ya Burundi.
Mazingira ya kamati kufika nyumbani kwa mganga huyo yalikuwa kama sinema ambapo wajumbe wa kamati wakiwa na askari polisi, baada ya kukaribia nyumba yake mganga akiwa ameshika mzizi mkononi na kibuyu kilichofungwa hirizi, aliwapa ishara ya kutosogelea nyumba hiyo.
“Wakati tukiwa mbele yake tukimfuata, alituambia tusisogelee nyumba yake kwani uchawi alionao una nguvu kubwa hivyo unaweza kutudhuru, hatukumsikiliza tuliendelea kumfuata hivyo alitupa vifaa vyake chini na kukimbilia ndani.
“Baadhi yetu walikuwa waoga katika eneo husika wakiogopa kudhurika, alipoingia ndani, alitokea mlango wa nyuma na kukimbia na sisi baada ya kuingia ndani, tulichukua vifaa vyake kama ushahidi,” alisema Bw. Mwamotto.
Aliongeza kuwa, kikosi kazi alichokiongoza kiliamua kwenda nyumbani kwa mganga huyo kwa lengo la kumkamata kutokana na malalamiko waliyopata kutoka kwa wateja wake ambao walidai kutumia fedha nyingi kumpa mtaalamu huyo hivyo walitaka kurudishiwa fedha zao.
Alisema baada ya kuzipasua hirizi walizozikuta, vibuyu na pembe, walikuta dawa za kienyeji pamoja na chura wazima wanaopumua. Vitu vingine walivyovikuta ni vitambaa vyeusi, vyeupe, vyekundu na vitu vingine vya ajabu.
Akizungumzia operesheni hiyo wilayani humo, alisema wamefanikiwa kukamata sare za Jeshi la Burundi na kofia vilivyokuwa vikitumika katika matukio mbalimbali ya uhalifu na wahamiaji haramu.“Tunaendelea na operesheni yetu kwa kushirikiana na viongozi ili kuhakikisha wahamiaji wote haramu wanarejeshwa nchini mwao tuweze kurudisha amani na usalama,” alisema.
Awali Mkuu wa Mkoa huo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama Mkoa, Issa Machibya, alisema wahamiaji haramu wengi walikuwa wakijihusisha na matukio ya ujangili na biashara ya silaha zikiwemo za kivita.
Alisema Mkoa huo pekee umewakamata wahamiaji haramu 4,365 kutoka nchini Burundi katika awamu ya kwanza ya operesheni iliyosambaa katika mikoa mbalimbali nchini na kuwataka wakazi wa Kigoma, kushiriki kikamilifu katika vita hiyo.
Kwa mujibu wa kiongozi wa timu ya Habari na Mawasiliano ya Operesheni Kimbunga, Zamaradi Kawawa, alisema katika operesheni hiyo awamu ya pili iliyofanyika Mikoa ya Geita, Kigoma na Kagera, bunduki moja aina ya SMG, bastola moja, magobole 17 na risasi 115 zikiwemo za bunduki aina ya SMG 102 na 13 za bastola vilikamatwa.
Wahamiaji haramu waliokamatwa wengi wao ni kutoka nchi za Burundi ambapo raia wake 114 walikamatwa wakiishi nchini kinyume na sheria na raia 20 wa Rwanda ambao nao walikamatwa katika kipindi hicho
Majira.

No comments:

Post a Comment