Wednesday, October 2, 2013

ALIYEKUFA AKIWA NA MADAWA YA KULEVYA TABATA...CHANZO NI KUTOA MADAWA YA KULEVYA TUMBONI KWA NJIA YA HAJA KUBWA


SIRI nzito imefumuka na ukweli kuanikwa baada ya Rajabu Kandunda, 43, mkazi wa Kigogo Luhanga kufariki dunia wiki iliyopita jijini Dar es Salaam akiwa na madawa ya kulevya tumboni.
Marehemu Rajabu Kandunda enzi za uhai wake. Uchunguzi umebaini kwamba, Kandunda alifariki dunia wakati akitoa madawa kwa njia ya haja kubwa nyumbani kwa rafiki yake aitwaye Nassiri Omari Rajabu maeneo ya Tabata Mawenzi, jijini Dar es Salaam.
Hii ndiyo nyumba alipofia Rajabu Kandunda. Uchunguzi unaonyesha kwamba marehemu aliondoka jijini Dar es Salaam Septemba 19, mwaka huu kwenda nchini Malawi huku akiwa amemeza madawa tumboni aina ya heroine lakini alipofika Newala, mkoani Mtwara akawa amelemewa na mzigo, hivyo kuamua kufupisha safari.
Habari kutoka kwa mtu wa karibu wa Kandunda zinadai kwamba, baada ya kuona amezidiwa aliwapigia simu ndugu zake kuwaarifu juu ya kuzidiwa kwake ambapo mkewe aitwaye Mwanaisha Salim,36, Nassiri Omari,36, na Doto Omari waliondoka Dar es Salaam Septemba 20 na kumfuata Newala.
Rafiki wa marehemu, Nassiri Omari Rajabu. “Pamoja na marehemu kuwa na hali mbaya kiafya lakini wanandugu hao walipofika Dar, hawakumfikishia hospitali wala nyumbani kwake Kigogo Luhanga bali walimsafirisha hadi kwa Nassiri, Tabata Mawenzi, kilisema chanzo hicho.
Habari zinadai kuwa alipofika hapo alipoenda chooni , baada ya muda mfupi akawa amefariki dunia wakati akitoa dawa kwa njia ya haja kubwa.
Chanzo hicho makini kilieleza kwamba marehemu alishaanza kutoa madawa lakini pumzi zilimuishia ghafla na kufia chooni ndipo Doto na mke wa marehemu wakaondoka kwenda Kigogo kuandaa utaratibu wa msiba.
Hata hivyo, inaelezwa kwamba kutokana na kifo hicho cha utata, Doto anadaiwa kutoweka na hajulikani alipo na jeshi la polisi linamsaka kwa udi na uvumba.

Imeelezwa kuwa mara baada ya marehemu kufariki dunia mmoja wa wanandugu aliwatonya polisi kuhusiana na kifo hicho na ilipofika saa 2.00 usiku askari walitinga nyumbani kwa Nassiri na kumkamata.
Polisi pia walimfuatilia mke wa marehemu aliyekwenda Kigogo na kumtia mbaroni, hadi leo watu hao wapo mikononi mwa polisi kwa uchunguzi.
Polisi walichukua mwili wa marehemu hadi Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa uchunguzi na daktari alipopasua tumbo lake walikuta madawa aina ya heroine pipi 33.
Hata hivyo, imeelezwa na mmoja wa wanafamilia kwamba marehemu aliwahi kufungwa mwaka 2008 huko Dubai baada ya kukutwa na madawa na alimaliza kifungo chake Agosti mwaka huu na kabla hajamaliza hata mwezi mauti yakamkuta.
Taarifa za kipolisi zinaeleza kwamba mke wa marehemu alipoulizwa kwamba kipindi cha nyuma mumewe alikuwa wapi, alieleza kuwa tangu mwaka 2004 alitoweka nyumbani na hakumuaga alikoenda hadi alipooneka Agosti mwaka huu.
Taarifa zaidi zinapasha kwamba, mkewe alieleza Septemba 19, mwaka huu mumewe alimuaga kwamba alikua anaenda Nairobi na hakumweleza anachofuata na alishangaa kusikia kuwa yupo Newala anaumwa.
Mwenye nyumba anayoishi Nassiri, Gidion Mpuya alipohojiwa alisema kwamba siku hiyo ya kifo hicho alifika nyumbani kwake saa 2.00 usiku na kuwakuta polisi nje ya geti kuu na hakujua kilichotokea.
“Nilipoingia chumbani kwangu mke wangu alinieleza kwamba kuna mtu kafariki kwa Nassiri na haikuchukua muda nikaona gari la polisi linaingia kuchukua mwili, Nassiri na mkewe wakashikiliwa na polisi.
“Hakukuwa na mtu wa kumuulizia kwa Nassiri bali nilipotoka nje majirani walinieleza kwamba mtu huyo kafariki na madawa tumboni.
“Nassiri ana zaidi ya miaka miwili na nusu tangu ahamie hapa, alikuwa akiishi na mkewe baadaye walikorofishana na zaidi ya miezi miwili hakuwepo hapo nyumbani,” alisema Mpuya.
Aliongeza kuwa mke wa Nassiri alirudi siku chache kabla ya marehemu kuja hapo kwao na yeye amekuwa akiwaona wageni wake wakifika na kuondoka lakini hakujua ujio wa marehemu kwani siku hiyo alifika na hakumalizika hata saa mmoja akafariki dunia.
Kamanda wa Polisi wa Kitengo cha Kupambana na Kudhibiti Madawa ya Kulevya nchini, Kamishna Mwandamizi, Godfrey Nzowa katika mahojianoi amesema kwamba wanamshikilia Nassiri na mke wa marehemu.
“Tunaendelea kumtafuta Doto, uchunguzi unaendelea na utakapokamilika hatua za kisheria zitachukuliwa kwa wale watakaopatikana na hatia,” alisema Nzowa.

No comments:

Post a Comment