Thursday, April 10, 2014

TAARIFA NA LUGHA SAHIHI: DHANA YA KUPUNGUZA MADHARA YA MAAFA

Meneja wa kituo cha Kahama FM Redio, Marco Mipawa, akiwakaribisha washiriki na kufungua warsha ya mafunzo ya siku nne ya waandishi wa habari na watangazaji wa Redio Jamii kuhusu kuandika taarifa za Maafa na Misaada ya Kibinadamu yanayofanyika mjini Kahama. Kushoto ni Mkufunzi wa Redio Jamii kutoka UNESCO Mama Rose Haji Mwalimu na kulia ni Hellen Msemo kutoka Mamamlaka ya Hali ya Hewa nchini (TMA).

Na Mwandishi Wetu

Ukosefu wa taarifa na lugha sahihi halikadhalika kukosa uelewa katika jamii ni miongoni mwa mambo yanayosababisha kutokea kwa maafa.

Katika mada inayohusu Misaada ya Kibinadamu na Taarifa za Maafa katika mafunzo ya siku nne ya wanahabari na watangazaji wa redio jamii mjini Kahama Mratibu wa idara ya Maafa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Bwana Harrison Christopher Chinyuka alisema jamii lazima ifahamu historia ya maeneo yanapotokea maafa na wapate elimu ya kutosha ili waweze kuepusha maafa asili.

Bwana Chinyuka alisema kwamba hilo litafanikiwa iwapo waandishi wa habari watawajibika kikamilifu kwa kuandika taarifa za majanga na maafa ambazo ni sahihi na kwa wakati kwa sababu wakati mwingine wamekuwa wakishindwa kutumia lugha sahihi ya kusheheneza taarifa husika. 
Mratibu wa Idara ya Maafa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Bwana Harrison Christopher Chinyuka Chinyuka, akiendesha mafunzo kwa waandishi na watangazaji wa Redio za Jamii nchini.

“Wanahabari wana mchango mkubwa katika kuhakikisha kuwa madhara ya maafa yanapunguzwa kwa kuipa uelewa jamii husika kwa kutoa taarifa na lugha sahihi zinazohusu maafa ili kutoa nafasi kwa wahanga kujihami ipasavyo”, alisema Bwana Chinyuka.

Wajibu wa mwandishi wa habari katika kupunguza maafa ni kukuza uelewa wa jamii kuhusu hatua za hatari, kuzuia na kukabiliana na maafa, kukubaliana juu ya viwango vya taratibu za uendeshaji katika sehemu ya maafa.

Wajibu mwingine ni kusambaza ujumbe wa onyo kwa kuaminika na haraka iwezekanavyo na kuiweka jamii vizuri kitaarifa wakati huo huo kuepuka uvumi na hofu katika hali ya hadhari.
Mkufunzi wa Redio Jamii kutoka UNESCO Mama Rose Haji Mwalimu, akihamaisha washiriki katika vikundi kazi.

“Wajibu wenu waandishi wa habari kabla, wakati na baada ya maafa ni kutimiza jukumu la kulinda na kusaidia kuunganisha familia na kujenga kujiamini, sio kuachia mchakato njiani”, alisema Bwana Chinyuka.

Madhumuni ya mafunzo hayo ni kutoa uwezo kwa waandishi wa habari na watangazaji wa redio jamii kuandika taarifa zinazohusu kutoa msaada wa kibinadamu na kupunguza madhara yatokanayo na majanga na maafa nchini katika mradi unofadhiliwa na shirika la maendeleo ya Sweden (SIDA) kwa kushirikiana na UNESCO.

Mafunzo hayo yanatekeleza malengo ya UNESCO linalohusisha kuimarisha uwezo wa kukuza mazingira ya uhuru wa kujieleza kwa ajili ya maendeleo, kuendeleza demokrasia na utamaduni wa mazungumzo ya amani bila migogoro.
Hellen Msemo kutoka Mamamlaka ya Hali ya Hewa nchini (TMA), akifafanua jambo wakati wa mafunzo hayo.
Mwandishi na mtangazaji kutoka kituo cha Redio O.R.S FM ya Simanjiro, Julius Laizer, akichangia maoni wakati wa mafunzo hayo yaliyofadhiliwa na Shirika la Maendeleo la Sweden (SIDA) kwa kushirikiana na UNESCO.
Picha juu na chini ni sehemu ya washiriki wakifuatilia mafunzo hayo kwa umakini yaliyofadhiliwa na Shirika la Maendeleo la Sweden (SIDA) kwa kushirikiana na UNESCO.
Mafunzo yakiendelea.

No comments:

Post a Comment