Wednesday, October 10, 2012

RAIS MSTAAFU ALLY HASSANI MWINYI ATINGA KISUTU




RAIS Mstaafu wa Awamu ya Pili, Ali Hassan Mwinyi (pichani) jana alipanda kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam kutoa ushahidi katika kesi ya kuibiwa zaidi ya Sh37milioni.

Mwinyi anakuwa Rais mstaafu wa pili kupanda kizimbani katika historia ya Tanzania baada ya Mei 7, mwaka huu Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa kupanda kizimbani mahakamani hapo kutoa ushahidi katika kesi ya aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia, Profesa Costa Mahalu.

Katika kesi hiyo, Profesa Mahalu alikuwa anakabiliwa na tuhuma za uhujumu uchumi. Hata hivyo, Mahakama ilimwachia huru baada ya kumwona hana hatia.

Mzee Mwinyi alipanda kizimbani katika kesi namba 201 ya mwaka huu inayosikilizwa na Hakimu Mkazi, Geni Dudu kutoa ushahidi wa kuibiwa kiasi hicho cha fedha mtuhumiwa akiwa ni wakala wake, Abdallah Nassoro Mzombe (39) ambaye ni mfanyabiashara na mkazi wa Kinondoni Mkwajuni, Dar es Salaam.

Mzombe anadaiwa kumwibia Rais Mstaafu Mwinyi jumla ya Sh37,440,000 zikiwa ni kodi ya pango katika nyumba mbili anazomiliki.

Kabla ya kesi hiyo kuanza kusikilizwa, Rais Mwinyi aliingizwa chemba namba moja kwa ajili ya kuandaliwa na Wakili wa Serikali, Charles Anindo na wakati huo maofisa wanne wanaodaiwa kuwa ni wa Usalama wa Taifa wakizunguka nje ya mlango wa ofisi hiyo ya Mahakama.

Ilipofika saa 5:05 asubuhi, askari mmoja wa Magereza alimpandisha mshtakiwa huyo, Mzombe mahakamani hapo kwa ajili ya kusikiliza kesi yake.

Baada ya mshtakiwa huyo kupandishwa na waandishi wa habari wote waliokuwepo kwenye eneo hilo nao wakijiandaa kuingia mahakamani ili kusikiliza kesi hiyo, maofisa hao waliwazuia.
Kati ya maofisa hao wanne, mmoja ambaye jina lake halikuweza kufahamika aliwahoji waandishi kabla ya kuwazuia kuingia:

Swali: Mnakwenda wapi?
Jibu: Tunakwenda mahakamani.
Swali: Nyie ni akina nani?
Jibu: Waandishi wa habari 
Swali: Mmeambiwa kuna mahakama humu?
Jibu: Ndiyo hiyo ni mahakama.

Baada ya waandishi wa habari kujibu hivyo, ofisa huyo aliwazuia kuingia kwenye Mahakama hiyo akisema... “Msiingie huku hii haiwahusu.”

Baada ya kuambiwa hivyo waandishi wa habari walikaa nje hadi saa 6:21 Rais Mwinyi alipomaliza kutoa ushahidi wake na kuondoka mahakamani hapo.

Kwa mujibu wa kesi hiyo iliyofunguliwa mahakamani hapo kwa mara ya kwanza Agosti 21 mwaka huu, Mzombe anadaiwa kufanya makosa hayo kinyume na Kifungu cha 258 na 273 (b) (e) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu, Sura ya 16 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.

Ilidaiwa kuwa kati ya Januari Mosi, 2011 na Julai 2012, huko Mikocheni, Mzombe akiwa Wakala wa Rais huyo mstaafu, alimwibia Sh17,640,000 ambazo ni pato la kodi ya nyumba yake iliyopo eneo la Mikocheni Wilaya ya Kinondoni.

Iliendelea kudai kuwa kiasi hicho cha fedha ambacho Mzombe alimwibia Rais Mwinyi kilikuwa ni kodi ya pango la nyumba namba 481, iliyopo kwenye Kiwanja A huko Mikocheni ya mwaka 2011/2012 na 2012/2013.

Mbali na shtaka hilo, pia anadaiwa kuwa kati ya Januari Mosi, 2011 na Julai 10, mwaka huu huko Msasani Village Wilaya ya Kinondoni, mshtakiwa huyo alimwibia tena Rais huyo mstaafu Sh19,800,000 ambazo zilikuwa ni kodi ya nyumba.

Iliongezwa kudaiwa kuwa kiasi hicho cha fedha kilikuwa ni kodi ya pango la nyumba hiyo la mwaka 2011/2012 na 2012/2013.

No comments:

Post a Comment