Saturday, January 19, 2013

BALOZI IDDI AKUTANA NA RAIS AL KHAIMAH ZANZIBAR

Mwakilishi wa Kampuni ya Kimataifa ya Mafuta na Gesi kutoka Nchini Ras Al Khaimah, Kamal Ahaya, akizungumza na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi hapo VIP Salama Bwawani Mjini Zanzibar.
Uongozi wa Kampuni ya Kimataifa ya Mafuta na Gesi kutoka Nchini Ras Al Khaimah ukiongozwa na Bwana Kamal Ahaya ukibadilishana mawazo na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi katika hatua za awali za kuanza kutekeleza miradi saba ya Maendeleo na ustawi wa jamii Nchini.
*********************

Serikali ya Ras Al Khaimah iko mbioni kutekeleza miradi saba iliyojipangia kuifanya hapa Zanzibar katika harakati zake za Kusaidia miradi ya Kiuchumi, Maendeleo na Ustawi wa Jamii wa Wananchi wa Zanzibar.
Maamuzi yaliyofikiwa na Nchi hiyo kupitia Uongozi wa Kampuni ya Kimataifa ya Mafuta na Gesi Kutoka Nchini humo { CEO Rak Gas } ndani ya kipindi cha miezi miwili iliyopita sasa yameanza hatua za utekelezaji.
Mwakilishi wa Kampuni ya Kimataifa ya Mafuta na Gesi kutoka Nchini Ras Al Khaimah { Ceo Rak Gas } Bwana Kamal Ahaya alieleza hayo wakati akizungumza na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi hapo katika Ukumbi wa Watu maarufu { VIP } uliopo Salama Bwawani Mjini Zanzibar.
Bwana Kamal alisema uongozi wa Kampuni yake ambao upo Nchini kuanza hatua za utekelezaji wa mpango huo unakusudia kutekeleza miradi saba miongoni mwake likiwemo suala la Maji Safi, Ujenzi wa Hospitali moja kubwa ya kisasa pamoja na sekta ya Elimu.
Mwakilishi huyo wa Kamuni ya Kimataifa ya Mafuta na Gesi ya Ras Al Khaimah alifahamkisha kwamba miradi hiyo muhimu kwa ustawi wa Jamii itakwenda sambamba na wananchi wenye mazingira magumu kuwezeshwa kujitegemea kupitia Taasisi inayosimamia michango ya Nchi hiyo ya Al Rahma Charity.
“ Tumeamua katika jitihada zetu za kusaidia Wananachi wa Zanzibar kuanza na ile miradi muhimu zaidi katika jamii kama Afya, Elimu,Maji na kuwawezesha wananachi wenye mazingira magumu Kimaisha”. Alifafanua Bwana Kamal Ahaya.
Alielezea faraja yake kutokana na mapokezi mazuri aliyoyapata yeye na ujumbe wake ambayo yalimjengea mazingira muwafaka ya kuanza kukutana na washirika wakuu watakaohusika na miradi hiyo hapa Zanzibar.
Kwa upande wake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi aliishukuru Serikali ya Ras Al Khaimah kwa uwamuzi wake wa kutekeleza ahadi iliyotowa ambayo imonyesha mwanga wa matumaini kwa wananachi walio wengi hapa Nchini.
Balozi Seif alisema miradi iliyopendekezwa na kupewa msukumo katika utekelezaj iwa mpango huo itaweza kusaidia kupunguza au kuondosha kabisa matatizo yanayowasumbuwa Wananchi hasa Afya na Maji safi na Salama miradi inayoendelea kutoa changamoto kwa Jamii.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alisema Ras Al Khaimah imekuwa mshirika wa karibu na wa muda mrefu kwa Zanzibar katika jitihada za pamoja za kutafuta mbinu za kutatua kero zinazowasumbnuwa Wananchi.
Mwakilishi huyo wa Kampuni ya Kimataifa ya Mafuta na Gesi Bwana Kamal aliwahi kukutana na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akiambatana pia na Mshauri wa Mkuu wa Mfalme wa Ras Al Khaimah Bwana Salem Ali Mwezi Novemba Mwaka uliopita Mjini Dodoma.


Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
19/1/2013.

No comments:

Post a Comment