Tuesday, August 20, 2013

Mwanamke ajilipua kwa petroli baada ya mumuwe kuoa mke wa pili huko Geita.

MWANAMKE mmoja ambaye ni mkazi wa Kijiji cha Nyankumbu, Kata ya Kalangalala mkoani Geita amenusurika kifo baada ya kujimwagia mwilini mafuta ya petroli kisha kujilipua baada ya mumewe kuoa mke wa pili. 

Imeelezwa kuwa mwanamke huyo, Anastazia Kubezya (28) Agosti 8 mwaka huu aliamua kujimiminia petroli mwili mzima kabla ya kuchukua kiberiti na kujilipua, hali iliyosababisha akimbizwe katika Hospitali ya Geita alikolazwa katika wodi namba saba kwa matibabu.

Akizungumza na mwandishi wetu, Consolata Raphael ambaye ni dada wa majeruhi huyo alidai kuwa chanzo cha mdogo wake huyo kufikia hatua ya kutaka kutumia njia hiyo ya mkato kwa lengo la kujiua ni wivu wa mapenzi.

Consolata alisema: “Siku ya tukio shemeji yangu George Kubezya (mume wa majeruhi), alifika nyumbani kwa mdogo wangu wa kiume akidai kuwa mkewe huyo anatishia kujiua baada ya kuoa mke wa pili.

“Tukiwa tunaendelea kujadiliana mara alitokea mkewe Kubezya akiwa na viatu vya mwanaye mdogo akamkabidhi mdogo wetu mwingine aitwaye Rozalia akamwambia mpatie mwanaye kwa kuwa anaondoka na hajui atarudi lini.

“Baada ya kutamka maneno hayo aliondoka na niliwasiliana na ndugu yetu mwingine aitwaye Elizabeth aliyesema Anastanzia alipita kwake akiwa na chupa ikiwa na petroli na walipojaribu kumkimbiza alipotelea gizani.


“Kati ya saa 4 na saa 5 usiku Eliza na wenzake walisikia mtu akilia nje ya nyuma yao na baada ya kutoka nje walikuta Anastanzia akiwa tayari amekwisha jilipua moto, walipomhoji alidai amefanya hivyo ili afe kutokana na mumewe kumuolea mke mwenza na kumleta kwenye nyumba waliyoijenga yeye na mumewe,”alisema Consolata. 

Hata hivyo juhudi za kumpata mumewe kuzungumzia sakata hilo hazikuzaa matunda baada ya kile kilichoelezwa kuwa alitoroka muda mfupi baada ya kumfikisha mkewe hospitalini.

Mwandishi wetu alifika hospitalini hapo na kukuta mwanamke huyo aliyelazwa wodi namba nane akiwa anauguzwa chini ya ulinzi wa polisi ili akipona afikishwe mahakamani kwa kosa la kujaribu kujiua.

Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Wilaya ya Geita, Dk. Adam Sijaona akizungumzia hali ya majeruhi huyo alisema bado si nzuri na wanafanya mpango wa kumhamishia katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando iliyopo jijini M
wanza.

No comments:

Post a Comment