Thursday, October 17, 2013

LULU : " SITAKI KUOLEWA MUDA WA KUOLEWA HAUJAFIKA"

STAA wa sinema za Kibongo, Elizabeth Michael ‘Lulu’ amekataa kabisa suala la kuolewa kwa sasa akidai moyo wake haupo tayari kwa tendo hilo.

Lulu alifunguka hayo Jumatatu iliyopita katika kipindi cha Mkasi kinachorushwa kupitia Runinga ya East Africa ambacho humpa nafasi staa kuzungumzia mambo mbalimbali yanayohusu maisha yake na sanaa kwa jumla.

Wakati mahojiano hayo yakiendelea, mmoja wa watangazaji wa kipindi hicho anayefahamika kwa jina la Muba, alimtupia Lulu swali ambalo lilimtaka aeleze utayari wake endapo mtu akijitokeza na kutaka kumuoa.

“Sitaki kuolewa kwa sasa, muda wa kuolewa haujafikia. Ukifika nitafanya hivyo lakini kwa sasa sipo tayari kuolewa,” alisema Lulu.
Aidha, Lulu alikiri kuwa licha ya kutokuwa tayari kuolewa lakini amekuwa akipata usumbufu mkubwa wa kutongozwa na wanaume. Aliainisha kuwa alikuwa akitongozwa kabla na baada ya kutoka Segerea alipokuwa akishikiliwa kwa kesi ya kifo cha aliyekuwa mpenzi wake, marehemu Steven Kanumba.
“Watu wananitongoza sana, walikuwa wakifanya hivyo kabla hata sijaingia China (gerezani Segerea) na wameendelea kufanya hivyo hata baada ya kutoka,” alisema Lulu na kuongeza:
“Siwezi kuwakubalia sababu sipo tayari kuolewa kwa sasa…muda wa kufanya hivyo haujafika.”
Kuhusu suala la kudaiwa kutembea na bosi wa Kampuni ya Proin Promotion ambayo inamsimamia kisanii kwa sasa, Lulu aliruka viunzi na kudai taasisi hiyo inamlea kama mtoto wa familia na siyo vinginevyo.
Alisema hata madai yanayoelekezwa kwake kuwa Proin wamempa gari na nyumba kama sehemu ya kuhongwa na bosi wa kampuni hiyo, hayana ukweli wowote kwani yeye anafanya kazi kama msanii chini ya kampuni hiyo na hakuna kitu cha ziada.
“Hahahaha! Salama (mtangazaji) acha mambo yako bwana… mimi nipo chini ya Proin kwa sasa kwa kipindi flani ambacho nimesaini nao mkataba. Wananilea kama msanii wao, hakuna cha ziada,” alisema Lulu.

Akiendelea kubwabwaja maneno ndani ya kipindi hicho, Lulu aliweka wazi kuwa alikuwa akishindwa kuanika penzi lake na marehemu Kanumba kwa kuwa muda muafaka ulikuwa haujafika na kudai waliishi kama mtu na baba yake kabla hawajawa wapenzi, wakawa wapenzi na mauti yakamkuta Kanumba kabla hawajalianika penzi lao.

No comments:

Post a Comment